41. Fussilat - Qurani
- 1. H`a Mim
- 2. Uteremsho huu umetoka kwa Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.
- 3. Hichi ni Kitabu kilicho pambanuliwa Aya zake, cha kusomwa kwa Kiarabu kwa watu wanao jua.
- 4. Kitoacho khabari njema, na chenye kuonya. Lakini wengi katika wao wamepuuza; kwa hivyo hawasikii.
- 5. Na wakasema: Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayo tuitia, na masikio yetu yana uziwi, na baina yetu na wewe lipo pazia. Basi wewe tenda, nasi tunatenda.
- 6. Sema: Hakika mimi ni mtu kama nyinyi; inafunuliwa kwangu ya kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu. Basi nyookeni sawa kumwendea Yeye, na mumtake msamaha, na ole wao wanao mshirikisha,
- 7. Ambao hawatoi Zaka na wanaikataa Akhera.
- 8. Hakika wanao amini na wakatenda mema watakuwa na ujira usio na ukomo.