logo HARUN YAHYA

An-Nazi`at - QURAN - Harun Yahya

  • 1. Naapa kwa wanao komoa kwa nguvu,
  • 2. Na kwa wanao toa kwa upole,
  • 3. Na wanao ogelea,
  • 4. Wakishindana mbio,
  • 5. Wakidabiri mambo.
  • 6. Siku kitapo tetemeka cha kutetemeka,
  • 7. Kifuate cha kufuatia.
  • 8. Siku hiyo nyoyo zitapiga piga,
  • 9. Macho yatainama chini.
  • 10. Sasa wanasema: Ati kweli tutarudishwa kwenye hali ya kwanza?
  • 11. Hata tukiwa mifupa iliyo bunguliwa?
  • 12. Wanasema: Basi marejeo hayo ni yenye khasara!
  • 13. Kwa hakika hayo ni ukelele mmoja tu,
  • 14. Mara watakuwa kwenye uwanda wa mkutano!
  • 15. Je! Imekufikia hadithi ya Musa?
  • 16. Mola wake Mlezi alipo mwita katika bonde takatifu la T`uwaa, akamwambia:
  • 17. Nenda kwa Firauni. Hakika yeye amezidi jeuri.
  • 18. Umwambie: Je! Unapenda kujitakasa?
  • 19. Nami nitakuongoa ufike kwa Mola wako Mlezi, upate kumcha.
  • 20. Basi alimwonyesha Ishara kubwa.
  • 21. Lakini aliikadhibisha na akaasi.
  • 22. Kisha alirudi nyuma, akaingia kufanya juhudi.
  • 23. Akakusanya watu akanadi.
  • 24. Akasema: Mimi ndiye Mola wenu Mlezi mkuu kabisa.
  • 25. Basi hapo Mwenyezi Mungu akamshika kumuadhibu kwa la mwisho na la mwanzo.
  • 26. Kwa hakika katika haya yapo mazingatio kwa wanao ogopa.
  • 27. Je! Ni vigumu zaidi kukuumbeni nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliye ijenga!
  • 28. Akainua kimo chake, na akaitengeneza vizuri.
  • 29. Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana wake.
  • 30. Na juu ya hivyo ameitandaza ardhi.
  • 31. Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake,
  • 32. Na milima akaisimamisha,
  • 33. Kwa nafuu yenu na mifugo yenu.
  • 34. Basi itakapo fika hiyo balaa kubwa,
  • 35. Siku ambayo mtu atakumbuka aliyo yafanya,
  • 36. Na Jahannamu itadhihirishwa kwa mwenye kuona,
  • 37. Basi ama yule aliye zidi ujeuri,
  • 38. Na akakhiari maisha ya dunia,
  • 39. Kwa hakika Jahannamu ndiyo makaazi yake!
  • 40. Na ama yule anaye ogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi, na akajizuilia nafsi yake na matamanio,
  • 41. Basi huyo, Pepo itakuwa ndiyo makaazi yake!
  • 42. Wanakuuliza Saa (ya Kiyama) itakuwa lini?
  • 43. Una nini wewe hata uitaje?
  • 44. Kwa Mola wako Mlezi ndio mwisho wake.
  • 45. Kwa hakika wewe ni mwonyaji tu kwa mwenye kuikhofu.
  • 46. Ni kama kwamba wao siku watapo iona (hiyo Saa) hawakukaa ila jioni moja tu, au mchana wake.
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code