logo HARUN YAHYA

Adh-Dhariyat - QURAN - Harun Yahya

  • 1. Naapa kwa pepo zinazo tawanya,
  • 2. Na zinazo beba mizigo,
  • 3. Na zinazo kwenda kwa wepesi.
  • 4. Na zinazo gawanya kwa amri,
  • 5. Hakika mnayo ahidiwa bila ya shaka ni kweli,
  • 6. Na kwa hakika malipo bila ya shaka yatatokea.
  • 7. Naapa kwa mbingu zenye njia,
  • 8. Hakika nyinyi bila ya shaka mmo katika kauli inayo khitalifiana.
  • 9. Anageuzwa kutokana na haki mwenye kugeuzwa.
  • 10. Wazushi wameangamizwa.
  • 11. Ambao wameghafilika katika ujinga.
  • 12. Wanauliza: Ni lini hiyo siku ya malipo?
  • 13. Hiyo ni siku watakayo adhibiwa Motoni.
  • 14. Onjeni adhabu yenu! Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyahimiza.
  • 15. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na chemchem.
  • 16. Wanapokea aliyo wapa Mola wao Mlezi. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema.
  • 17. Walikuwa wakilala kidogo tu usiku.
  • 18. Na kabla ya alfajiri wakiomba maghfira.
  • 19. Na katika mali yao ipo haki ya mwenye kuomba na asiye omba.
  • 20. Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini.
  • 21. Na pia katika nafsi zenu - Je! Hamwoni?
  • 22. Na katika mbingu ziko riziki zenu na mliyo ahidiwa.
  • 23. Basi naapa kwa Mola Mlezi wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo kweli kuwa nyinyi mnasema.
  • 24. Je! Imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanao hishimiwa?
  • 25. Walipo ingia kwake wakasema: Salama! Na yeye akasema: Salama! Nyinyi ni watu nisio kujueni.
  • 26. Akenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliye nona.
  • 27. Akawakaribisha, akasema: Mbona hamli?
  • 28. Akahisi kuwaogopa katika nafsi yake. Wakasema: Usiwe na khofu, nao wakambashiria kupata kijana mwenye ilimu.
  • 29. Ndipo mkewe akawaelekea, na huku anasema na akijipiga usoni kwa mastaajabu, na kusema: Mimi ni kikongwe na tasa!
  • 30. Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyo sema Mola wako Mlezi. Hakika Yeye ni Mwenye hikima na Mwenye kujua.
  • 31. AKASEMA: Basi ujumbe wenu ni nini, enyi mlio tumwa?
  • 32. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa watu wakosefu,
  • 33. Tuwatupie mawe ya udongo,
  • 34. Yaliyo tiwa alama kutoka kwa Mola wako Mlezi kwa ajili ya wanao pindukia mipaka.
  • 35. Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walio amini.
  • 36. Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu!
  • 37. Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanao iogopa adhabu chungu.
  • 38. Na katika khabari za Musa, tulipo mtuma kwa Firauni na hoja wazi.
  • 39. Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake na akasema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu!
  • 40. Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa.
  • 41. Na katika khabari za A`di tulipo wapelekea upepo wa kukata uzazi.
  • 42. Haukuacha chochote ulicho kifikia ila ulikifanya kama kilio nyambuka.
  • 43. Na katika khabari za Thamudi walipo ambiwa: Jifurahisheni kwa muda mdogo tu.
  • 44. Wakaasi amri ya Mola wao Mlezi. Basi uliwanyakua moto wa radi nao wanaona.
  • 45. Basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea.
  • 46. Na kaumu ya Nuhu hapo mbele. Hakika hao walikuwa watu wapotovu.
  • 47. Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio twenye uwezo wa kuzitanua.
  • 48. Na ardhi tumeitandaza; basi watandazaji wazuri namna gani Sisi!
  • 49. Na katika kila kitu tumeumba kwa jozi ili mzingatie.
  • 50. Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.
  • 51. Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.
  • 52. Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu.
  • 53. Je! Wameambizana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi.
  • 54. Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi.
  • 55. Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini.
  • 56. Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi.
  • 57. Na sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe.
  • 58. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti.
  • 59. Hakika walio dhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao. Basi wasinihimize.
  • 60. Ole wao walio ikanusha siku yao waliyo ahidiwa.
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code