logo HARUN YAHYA

Al-Insan - QURAN - Harun Yahya

  • 1. Hakika kilimpitia binaadamu kipindi katika zama ambacho kwamba hakuwa kitu kinacho tajwa.
  • 2. Hakika Sisi tumemuumba mtu kutokana na mbegu ya uhai iliyo changanyika, tumfanyie mtihani. Kwa hivyo tukamfanya mwenye kusikia, mwenye kuona.
  • 3. Hakika Sisi tumembainishia Njia. Ama ni mwenye kushukuru, au mwenye kukufuru.
  • 4. Hakika Sisi tumewaandalia makafiri minyororo na pingu na Moto mkali.
  • 5. Hakika watu wema watakunywa katika vinywaji vilivyo changanyika na kafuri,
  • 6. Ni chemchem watakao inywa waja wa Mwenyezi Mungu, wakiifanya imiminike kwa wingi.
  • 7. Wanatimiza ahadi, na wanaiogopa siku ambayo shari yake inaenea sana,
  • 8. Na huwalisha chakula, juu ya kukipenda kwake, masikini, na yatima, na wafungwa.
  • 9. Hakika sisi tunakulisheni kwa wajihi wa Mwenyezi Mungu. Hatutaki kwenu malipo wala shukrani.
  • 10. Hakika sisi tunaiogopa kwa Mola wetu Mlezi hiyo siku yenye shida na taabu.
  • 11. Basi Mwenyezi Mungu atawalinda na shari ya siku hiyo, na atawakutanisha na raha na furaha.
  • 12. Na atawajazi Bustani za Peponi na maguo ya hariri kwa vile walivyo subiri.
  • 13. Humo wataegemea juu ya viti vya enzi, hawataona humo jua kali wala baridi kali.
  • 14. Na vivuli vyake vitakuwa karibu yao, na mashada ya matunda yataning`inia mpaka chini.
  • 15. Na watapitishiwa vyombo vya fedha na vikombe vya vigae,
  • 16. Vya fedha safi kama kiyoo, wamevipima kwa vipimo.
  • 17. Na humo watanyweshwa kinywaji kilicho changanyika na tangawizi.
  • 18. Hiyo ni chemchem iliyo humo inaitwa Salsabil.
  • 19. Na watawazungukia kuwatumikia wavulana wasio pevuka, ukiwaona utawafikiri ni lulu zilizo tawanywa.
  • 20. Na utakapo yaona, utakuwa umeona neema na ufalme mkubwa.
  • 21. Juu yao zipo nguo za hariri laini za kijani kibichi, na hariri nzito ya at`ilasi. Na watavikwa vikuku vya fedha, na Mola wao Mlezi atawanywesha kinywaji safi kabisa.
  • 22. Hakika haya ni malipo yenu; na juhudi zenu zimekubaliwa.
  • 23. Hakika Sisi tumekuteremshia Qur`ani kidogo kidogo.
  • 24. Basi ngojea hukumu ya Mola wako Mlezi wala usimt`ii miongoni mwao mwenye dhambi au mwenye kufuru.
  • 25. Na likumbuke jina la Mola wako Mlezi asubuhi na jioni;
  • 26. Na usiku msujudie Yeye, na umtakase usiku, wakati mrefu.
  • 27. Kwa hakika watu hawa wanapenda maisha ya kidunia, na wanaiacha nyuma yao siku nzito.
  • 28. Sisi tumewaumba, na tukavitia nguvu viungo vyao. Na tukitaka tutawabadilisha mfano wao wawe badala yao.
  • 29. Hakika haya ni mawaidha; basi anaye taka atashika Njia ya kwenda kwa Mola wake Mlezi.
  • 30. Wala hamwezi kutaka ila atakapo Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye ilimu, Mwenye hikima.
  • 31. Humuingiza amtakaye katika rehema yake. Na wenye kudhulumu amewawekea adhabu iliyo chungu.
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code