logo HARUN YAHYA

Al-Qamar - QURAN - Harun Yahya

  • 1. Saa imekaribia, na mwezi umepasuka!
  • 2. Na wakiona Ishara hugeuka upande na husema: Huu uchawi tu unazidi kuendelea.
  • 3. Na wamekanusha na wamefuata matamanio yao. Na kila jambo ni lenye kuthibiti.
  • 4. Na bila ya shaka zimewajia khabari zenye makaripio.
  • 5. Hikima kaamili; lakini maonyo hayafai kitu!
  • 6. Basi jiepushe nao. Siku atakapo ita mwitaji kuliendea jambo linalo chusha;
  • 7. Macho yao yatainama; watatoka makaburini kama nzige walio tawanyika,
  • 8. Wanamkimbilia mwitaji, na makafiri wanasema: Hii ni siku ngumu.
  • 9. Kabla yao kaumu ya Nuhu walikanusha; wakamkanusha mja wetu, na wakasema ni mwendawazimu, na akakaripiwa.
  • 10. Basi akamwomba Mola wake Mlezi akasema: Kwa hakika mimi nimeshindwa, basi ninusuru!
  • 11. Basi tukaifungua milango ya mbingu kwa maji yanayo miminika.
  • 12. Na tukazipasua ardhi kwa chemchem, yakakutana maji kwa jambo lilio kadiriwa.
  • 13. Na tukamchukua kwenye safina ya mbao na kamba.
  • 14. Ikawa inakwenda kwa nadhari yetu, kuwa ni malipo kwa alivyo kuwa amekanushwa.
  • 15. Na bila ya shaka tuliiacha iwe ni Ishara. Lakini je, yupo anaye kumbuka?
  • 16. Basi ilikuwaje adhabu yangu, na maonyo yangu.
  • 17. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur`ani iwe nyepesi kufahamika. Lakini yupo anaye kumbuka?
  • 18. Kina A`di walikanusha. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?
  • 19. Hakika Sisi tuliwapelekea upepo wa kimbunga katika siku korofi mfululizo,
  • 20. Ukiwang`oa watu kama vigogo vya mitende vilio ng`olewa.
  • 21. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu?
  • 22. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur`ani nyepesi kufahamika; lakini yupo anaye kumbuka?
  • 23. Thamudi waliwakanusha Waonyaji.
  • 24. Wakasema: Ati tumfuate binaadamu mmoja katika sisi? Basi hivyo sisi tutakuwa katika upotofu na kichaa!
  • 25. Ni yeye tu aliye teremshiwa huo ukumbusho kati yetu sote? Bali huyu ni mwongo mwenye kiburi!
  • 26. Kesho watajua ni nani huyo mwongo mwenye kiburi.
  • 27. Hakika Sisi tutawapelekea ngamia jike ili kuwajaribu, basi watazame tu na ustahamili.
  • 28. Na waambie kwamba maji yatagawanywa baina yao; kila sehemu ya maji itahudhuriwa na aliye khusika.
  • 29. Basi wakamwita mtu wao akaja akamchinja.
  • 30. Basi ilikuwaje adhabu yangu na maonyo yangu!
  • 31. Hakika Sisi tuliwapelekea ukelele mmoja tu, wakawa kama mabuwa ya kujengea uwa.
  • 32. Na bila ya shaka Sisi tumeifanya Qur`ani iwe nyepesi kwa kukumbuka, lakini yupo akumbukaye?
  • 33. Kaumu Lut`i nao waliwakadhibisha Waonyaji.
  • 34. Hakika Sisi tukawapelekea kimbunga cha vijiwe, isipo kuwa wafuasi wa Lut`i. Hao tuliwaokoa karibu na alfajiri.
  • 35. Kwa neema inayo toka kwetu. Hivyo ndivyo tumlipavyo anaye shukuru.
  • 36. Na hakika yeye aliwaonya adhabu yetu; lakini wao waliyatilia shaka hayo maonyo.
  • 37. Na walimtaka awape wageni wake. Tukayapofua macho yao, na tukawaambia: Onjeni basi adhabu na maonyo yangu!
  • 38. Na iliwafikia wakati wa asubuhi adhabu yangu ya kuendelea.
  • 39. Basi onjeni adhabu na maonyo yangu!
  • 40. Na hakika tumeisahilisha Qur`ani kuikumbuka. Lakini yupo anaye kumbuka?
  • 41. Na Waonyaji waliwafikia watu wa Firauni.
  • 42. Walizikadhibisha Ishara zetu zote, nasi tukawashika kama anavyo shika Mwenye nguvu Mwenye uweza.
  • 43. Je! Makafiri wenu ni bora kuliko hao, au yameandikwa vitabuni kuwa nyinyi hamtiwi makosani?
  • 44. Au ndio wanasema: Sisi ni wengi tutashinda tu.
  • 45. Wingi wao huu utashindwa, na wao watasukumwa nyuma.
  • 46. Bali Saa ya Kiyama ndio miadi yao, na Saa hiyo ni nzito zaidi na chungu zaidi.
  • 47. Hakika wakosefu wamo katika upotofu na wazimu.
  • 48. Siku watakapo kokotwa Motoni kifudifudi waambiwe: Onjeni mguso wa Jahannamu!
  • 49. Kwa hakika Sisi tumekiumba kila kitu kwa kipimo.
  • 50. Na amri yetu haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho.
  • 51. Na bila ya shaka tumekwisha waangamiza wenzenu. Lakini yupo anaye kumbuka?
  • 52. Na kila jambo walilo lifanya limo vitabuni.
  • 53. Na kila kidogo na kikubwa kimeandikwa.
  • 54. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani na mito.
  • 55. Katika makalio ya haki kwa Mfalme Mwenye uweza.
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code