logo HARUN YAHYA

Ad-Dukhan - QURAN - Harun Yahya

  • 1. H`a Mim
  • 2. Naapa kwa Kitabu kinacho bainisha,
  • 3. Hakika tumekiteremsha katika usiku ulio barikiwa. Hakika Sisi ni Waonyaji.
  • 4. Katika usiku huu hubainishwa kila jambo la hikima,
  • 5. Jambo litokalo kwetu. Hakika Sisi ndio wenye kutuma.
  • 6. Ni rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia Mwenye kujua.
  • 7. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilio baina yao, ikiwa nyinyi mna yakini.
  • 8. Hakuna mungu ila Yeye; anahuisha na anafisha- Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa baba zenu wa mwanzo.
  • 9. Lakini wao wanacheza katika shaka.
  • 10. Basi ingoje siku ambayo mbingu zitakapo leta moshi ulio dhaahiri,
  • 11. Utakao wafunika watu: Hii ni adhabu chungu!
  • 12. Mola wetu Mlezi! Tuondolee adhabu hii. Hakika tutaamini.
  • 13. Nini faida ya kukumbuka kwao? Na alikwisha wafikia Mtume mwenye kubainisha.
  • 14. Na wao wakamgeuzia uso, na wakasema: Huyu amefunzwa, naye ni mwendawazimu.
  • 15. Hakika sisi tutaiondoa adhabu kidogo, lakini nyinyi kwa yakini mtarejea vile vile!
  • 16. Siku tutayo yashambulia mashambulio makubwa, bila ya shaka Sisi ni wenye kutesa.
  • 17. Na hakika kabla ya hawa tuliwafanyia mtihani watu wa Firauni, na aliwafikia Mtume Mtukufu.
  • 18. Akasema: Nipeni waja wa Mwenyezi Mungu; kwa hakika mimi kwenu ni Mtume Muaminifu.
  • 19. Na msimfanyie kiburi Mwenyezi Mungu; hakika mimi nitakuleteeni uthibitisho ulio wazi.
  • 20. Nami najikinga kwa Mola wangu Mlezi na ndiye Mola wenu Mlezi pia, ili msinipige mawe.
  • 21. Na ikiwa hamniamini, basi jitengeni nami.
  • 22. Ndipo akamwomba Mola wake Mlezi: Hakika watu hawa ni wakosefu.
  • 23. Mwenyezi Mungu akasema: Basi nenda na waja wangu usiku. Kwa yakini mtafuatwa.
  • 24. Na iache bahari vivyo hivyo imeachana, hakika wao hao ni jeshi litakalo zamishwa.
  • 25. Mabustani mangapi, na chemchem ngapi waliziacha!
  • 26. Na mimea na vyeo vitukufu!
  • 27. Na neema walizo kuwa wakijistareheshea!
  • 28. Ndio hivyo! Na tukawarithisha haya watu wenginewe.
  • 29. La mbingu wala ardhi hazikuwalilia, wala hawakupewa muhula.
  • 30. Na bila ya shaka tuliwaokoa Wana wa Israili katika adhabu ya kuwadhalilisha,
  • 31. Ya Firauni. Hakika yeye alikuwa jeuri katika wenye kupindukia mipaka.
  • 32. Na tuliwakhiari kwa ujuzi wetu kuliko walimwengu wenginewe.
  • 33. Na tukawapa katika ishara zenye majaribio yaliyo wazi.
  • 34. Hakika hawa wanasema:
  • 35. Hapana ila kufa kwetu mara ya kwanza tu, wala sisi hatufufuliwi.
  • 36. Basi warudisheni baba zetu, ikiwa nyinyi mnasema kweli.
  • 37. Je! Ni wao bora au watu wa Tubbaa` na walio kuwa kabla yao? Tuliwaangamiza. Hakika hao walikuwa wakosefu.
  • 38. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo baina yake kwa mchezo.
  • 39. Hatukuviumba hivyo ila kwa Haki, lakini wengi wao hawajui.
  • 40. Hakika siku ya Uamuzi ni wakati ulio wekwa kwa wao wote.
  • 41. Siku ambayo rafiki hatamfaa rafiki yake kwa chochote, wala hawatanusuriwa.
  • 42. Isipo kuwa atakaye mrehemu Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
  • 43. Hakika Mti wa Zaqqum,
  • 44. Ni chakula cha mwenye dhambi.
  • 45. Kama shaba iliyo yayushwa, hutokota matumboni
  • 46. Kama kutokota kwa maji ya moto.
  • 47. (Itasemwa:) Mkamateni na mtupeni katikati ya Jahannamu!
  • 48. Kisha mmwagieni juu ya kichwa chake adhabu ya maji yanayo chemka.
  • 49. Onja! Ati wewe ndiye mwenye nguvu, mtukufu!
  • 50. Hakika haya ndiyo mliyo kuwa mkiyatilia shaka.
  • 51. Hakika wachamngu watakuwa katika mahali pa amani,
  • 52. Katika mabustani na chemchem,
  • 53. Watavaa hariri nyepesi na hariri nzito wakikabiliana,
  • 54. Hivi ndivyo itakavyo kuwa, na tutawaoza mahurilaini.
  • 55. Humo watataka kila aina ya matunda, na wakae kwa amani.
  • 56. Humo hawataonja mauti ila mauti yale ya kwanza, na (Mwenyezi Mungu) atawalinda na adhabu ya Jahannamu,
  • 57. Kuwa ni fadhila zitokazo kwa Mola wako Mlezi. Huko ndiko kufuzu kukubwa.
  • 58. Basi tumeifanya nyepesi hii Qur`ani kwa ulimi wako, ili wapate kukumbuka.
  • 59. Ngoja tu, na wao wangoje pia.
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code