logo HARUN YAHYA

An-Naba - QURAN - Harun Yahya

  • 1. WANAULIZANA nini?
  • 2. Ile khabari kuu,
  • 3. Ambayo kwayo wanakhitalifiana.
  • 4. La! Karibu watakuja jua.
  • 5. Tena la! Karibu watakuja jua.
  • 6. Kwani hatukuifanya ardhi kama tandiko?
  • 7. Na milima kama vigingi?
  • 8. Na tukakuumbeni kwa jozi?
  • 9. Na tukakufanya kulala kwenu ni mapumziko?
  • 10. Na tukaufanya usiku ni nguo?
  • 11. Na tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha?
  • 12. Na tukajenga juu yenu saba zenye nguvu?
  • 13. Na tukaifanya taa yenye mwanga na joto;
  • 14. Na tukateremsha maji yanayo anguka kwa kasi kutoka mawinguni,
  • 15. Ili tutoe kwayo nafaka na mimea,
  • 16. Na mabustani yenye miti iliyo kamatana.
  • 17. Hakika siku ya uamuzi imewekewa wakati wake,
  • 18. Siku litapo pulizwa barugumu, nanyi mtakuja kwa makundi,
  • 19. Na mbingu zitafunguliwa, ziwe milango,
  • 20. Na milima itaondolewa na itakuwa kama sarabi.
  • 21. Hakika Jahannamu inangojea!
  • 22. Kwa walio asi ndio makaazi yao,
  • 23. Wakae humo karne baada ya karne,
  • 24. Hawataonja humo chochote kibaridi wala kinywaji,
  • 25. Ila maji yamoto sana na usaha,
  • 26. Ndio jaza muwafaka.
  • 27. Hakika hao hawakuwa wakitaraji kuwa kuna hisabu.
  • 28. Na wakikanusha Aya zetu kwa nguvu.
  • 29. Na kila kitu Sisi tumekidhibiti kwa kukiandika.
  • 30. Basi onjeni! Nasi hatutakuzidishieni ila adhabu!
  • 31. Hakika wachamngu wanastahiki kufuzu,
  • 32. Mabustani na mizabibu,
  • 33. Na wake walio lingana nao,
  • 34. Na bilauri zilizo jaa,
  • 35. Hawatasikia humo upuuzi wala uwongo -
  • 36. Malipo kutoka kwa Mola wako Mlezi, kipawa cha kutosha.
  • 37. Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilio baina yao, Arrahman, Mwingi wa rehema; hawamiliki usemi mbele yake!
  • 38. Siku atakapo simama Roho na Malaika kwa safu. Hawatasema ila Mwingi wa rehema aliye mruhusu, na atasema yaliyo sawa tu.
  • 39. Hiyo ndiyo Siku ya haki. Basi anaye taka na ashike njia arejee kwa Mola wake Mlezi.
  • 40. Hakika tumekuhadharisheni adhabu iliyo karibu kufika; Siku ambayo mtu atakapo ona yaliyo tangulizwa na mikono yake; na kafiri atasema: Laiti ningeli kuwa udongo!
SHIRIKI
Facebook
X
WhatsApp
Telegram
QR Code
QR Code